Articles by "HABARI NA MATUKIO"
Showing posts with label HABARI NA MATUKIO. Show all posts
Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, IGP Camillus Wambura, amefungua rasmi mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Sekretarieti ya Maadili ya Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Dodoma, yanayofanyika katika Chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es Salaam (DPA) kuanzia tarehe 15 hadi 19 Disemba, 2025.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, IGP Wambura, alisisitiza kuwa. mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha watendaji kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uwajibikaji na uadilifu mkubwa zaidi ili kuendelea kutoa huduma bora kwa jamii.

Alibainisha kuwa, mafunzo hayo yataimarisha uwezo wa washiriki katika kusimamia maadili, kushughulikia malalamiko ya wananchi, kuandaa taarifa za robo mwaka na mwaka pamoja na kutumia kikamilifu Mfumo wa Kielektroniki wa Kushughulikia Mrejesho (e-Mrejesho) ili kuongeza uwazi na ufanisi ndani ya Jeshi la Polisi.

Aidha, IGP Wambura alisisitiza umuhimu wa maadili kwa viongozi, akieleza kuwa mmomonyoko wa maadili kwa viongozi wa juu huathiri mwenendo wa taasisi nzima na kuwataka washiriki kuwa mfano bora wa maadili mema ili kulinda taswira ya Jeshi la Polisi na kuendeleza imani ya wananchi kwa jeshi hilo.
Akihitimisha hotuba yake, IGP Wambura aliwataka washiriki kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyopo katika kushughulikia malalamiko, kupambana na vitendo vya rushwa na ukiukwaji wa maadili bila upendeleo, huku akieleza kuwa mafunzo hayo ni chachu ya kuimarisha Nidhamu, Haki, Weledi na Uadilifu ndani ya Jeshi la Polisi Tanzania.

Kwa upande wake, Kamishna wa Utawala na Menejimenti ya Rasilimali Watu wa Jeshi la Polisi, CP Tatu Jumbe, akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, alisema mafunzo hayo ni muhimu kwa kuwa yatalenga kuwajengea uwezo washiriki kutambua na kutekeleza kikamilifu majukumu ya Kamati ya Kusimamia Maadili na Ushughulikiaji wa Malalamiko pamoja na Watendaji wa Sehemu (Chiefdom) ya Maadili na Malalamiko.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali itachukua hatua kali za kisheria dhidi ya viongozi na watumishi wa umma watakaoshindwa kujaza na kuwasilisha kwa wakati fomu za tamko la maadili katika Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Rais Dkt. Mwinyi ametoa kauli hiyo leo wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu Zanzibar, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Dimani, Mkoa wa Mjini Magharibi. Amesisitiza kuwa kwa mujibu wa sheria, kila kiongozi na mtumishi wa umma anatakiwa kuwasilisha fomu hizo kabla ya tarehe 30 Desemba 2025.

Akielezea taarifa ya Mwenyekiti wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa hadi sasa ni viongozi 530 pekee, sawa na asilimia 19, kati ya viongozi 2,750 wanaotakiwa kisheria, ndio waliokamilisha zoezi hilo. Ameeleza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya watakaokiuka matakwa hayo ya kisheria.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali ipo katika maandalizi ya kuanzisha Mfumo wa Upimaji wa Utendaji Kazi kwa Viongozi, utakaolenga kuongeza uwajibikaji, ufanisi na tija katika utoaji wa huduma kwa wananchi pamoja na kuimarisha utendaji wa taasisi za umma.

Akizungumzia mapambano dhidi ya rushwa na uhujumu wa uchumi, Rais Dkt. Mwinyi amesema Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi (ZAECA) imepokea na kufanyia kazi jumla ya taarifa 524. Amefafanua kuwa katika kipindi cha Januari hadi Oktoba 2025, ZAECA imefanikiwa kidhibiti na kuokoa Jumla ya Shilingi 6,426,282,551/= na dola za kimarekani (USD) 89,371 zilirejeshwa Serikalini na shilingi 1,143,487,556/= na dola za Kimaekani (USD) 4,999 zilirejeshwa kwa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi amesema Tanzania, ikiwemo Zanzibar, imeendelea kupiga hatua kubwa katika utekelezaji wa Malengo ya Umoja wa Mataifa yanayohusiana na haki za binadamu na mapambano dhidi ya rushwa, kupitia uridhiaji na utekelezaji wa mikataba na mikakati ya kimataifa.
Akihitimisha hotuba yake, Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito kwa viongozi wa taasisi za Serikali kutumia vyombo vya habari kuwaelimisha wananchi kuhusu shughuli na maendeleo ya nchi, na pia kuhimiza wananchi, vyombo vya habari, asasi za kiraia na sekta ya umma kushirikiana na Serikali katika kuimarisha utawala bora, haki za binadamu na mapambano dhidi ya rushwa.

Vilevile, Rais Dkt. Mwinyi ameipongeza Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kushughulikia malalamiko ya wananchi kuhusu uvunjaji wa maadili ya viongozi, ambapo jumla ya malalamiko 28 yalipokelewa na manane tayari yamefanyiwa kazi.
Nairobi. Rais wa Jamhuri ya Kenya, Dkt. William Ruto, amemtunuku mwanaharakati wa mazingira Truphena Muthoni Medali ya Head of State Commendation (HSC) kwa mchango wake wa kipekee katika kuhamasisha uhifadhi wa mazingira na mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

Tuzo hiyo imetolewa kufuatia hatua ya kihistoria ya Muthoni ya kutumia saa 72 mfululizo akikumbatia mti wa asili, tukio lililovunja rekodi na kuvutia hisia za kitaifa na kimataifa kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira.
Rais Ruto alisema alifurahishwa na ujasiri, uthubutu na dhamira ya dhati aliyoionesha Muthoni, akieleza kuwa vitendo vyake vinaakisi roho ya uzalendo na uongozi unaohitajika katika kukabiliana na changamoto za mazingira.

“Hatua yake ni ujumbe mzito kwa dunia nzima kuhusu wajibu wetu wa kulinda mazingira kwa vizazi vijavyo,” alisema Rais Ruto.
Katika kutambua mchango huo, Rais amemteua Truphena Muthoni kuwa Balozi wa Kampeni ya Kitaifa ya Kupanda Miti Bilioni 15, mpango mahsusi wa serikali unaolenga kurejesha misitu na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi nchini Kenya.

Aidha, Shirika la Huduma za Wanyamapori Kenya (KWS) kwa kushirikiana na Bodi ya Utalii Kenya (KTB) limempa Muthoni pamoja na timu yake likizo iliyodhaminiwa kikamilifu kama sehemu ya kuthamini juhudi zake za kuhamasisha jamii.
Wakati huo huo, Wizara ya Mazingira, Mabadiliko ya Tabianchi na Misitu imetangaza kuunga mkono ndoto ya Muthoni ya kutembelea Brazil ili kupata uzoefu wa kimataifa kuhusu uhifadhi wa mazingira na uongozi wa kimazingira.

Hatua ya serikali kumuenzi Truphena Muthoni inaonesha dhamira ya Kenya ya kuwa mstari wa mbele katika mapambano ya kulinda mazingira, huku ikiendelea kuhimiza ushiriki wa vijana katika kulinda rasilimali za taifa.
Mkuu wa kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim Bw. Silas Matoi, akizungumza na mmoja wa washindi wakati wa droo ya kwanza ya kampeni ya Chanja Kijanja, Dili ndio Hili iliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita. Kupitia kampeni hii, wateja wanaotumia kadi za Exim kulipia bidhaa au huduma wanapata nafasi ya kushinda zawadi ya pesa taslimu TZS 100,000 kila wiki, TZS 200,000 kila mwezi, pamoja na zawadi kubwa za TZS milioni 15, milioni 10 na milioni 5 mwisho wa kampeni.Kushoto ni Meneja Msaidizi wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim Benedict Mwinula, pamoja na Mkaguzi kutoka Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania, Rodgers Biteko (kulia), jijini Dar es Salaam.
Droo ya kwanza ya kampeni ya Chanja Kijanja, Dili ndio Hili imeibua washindi watano wa Sh. 100,000 kila mmoja! Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim, Bw. Silas Matoi, aliwatangaza washindi huku akisisitiza kuwa hii ni mwanzo tu.

“Kila wiki, washindi watatangazwa, na kila mwezi washindi 10 watashinda Sh. 200,000. Vilevile, washindi wa droo kuu watapokea zawadi kubwa za Sh. milioni 5, milioni10, na mshindi mkuu Sh. milioni 15,” alisema Bw. Matoi.
Benedict Mwinula, Meneja Msaidizi wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali, pamoja na Rodgers Biteko, Mkaguzi kutoka Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania, walishiriki katika droo hii iliyofanyika mwishoni mwa wiki.

Kampeni ya Chanja Kijanja inalenga kuwapa wateja wa Exim fursa ya kushinda kila wanapotumia kadi za Exim kulipia bidhaa au huduma. Hii ni nafasi yako ya kuwa mmojawapo wa mshindi wa Sh. 15 milioni!
Na WMJJWM – Tunisia

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, ameshiriki Mkutano wa 6 wa Ngazi ya Juu kuhusu Masuala ya Wanawake, Amani na Usalama (WPS) uliofanyika tarehe 9–10 Desemba 2025 katika Chuo cha Kimataifa cha Diplomasia, jijini Tunis nchini Tunisia.

Akizungumza katika mkutano huo, Dkt. Gwajima ameupongeza Umoja wa Afrika kupitia Ofisi ya Mjumbe Maalum wa AU wa Masuala ya Wanawake, Amani na Usalama, pamoja na Serikali ya Tunisia kwa kuandaa mkutano huo muhimu wenye mstakabali wa Wanawake.

Akiwasilisha mchango wake katika mjadala wa jopo la wataalamu, Dkt. Gwajima amesema kasi ya ukuaji wa teknolojia na akili mnemba imekuwa na manufaa pale inapowezesha jamii kuelimishwa kuhusu madhara ya ukatili wa kijinsia, sambamba na kusambaza ujumbe wa kukataa vitendo hivyo.

Dkt. Gwajima pia ameeleza mafanikio makubwa yaliyofikiwa na Tanzania, ikiwemo kuzinduliwa kwa Mpango wa Taifa wa Kwanza wa Wanawake, Amani na Usalama (TNAP), mageuzi ya sera na sheria kama Sheria ya Uchaguzi ya 2024, pamoja na ongezeko la uwakilishi wa wanawake katika nafasi za maamuzi serikalini. Aidha, amebainisha hatua za serikali kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia mikopo ya asilimia 10 ya halmashauri na juhudi za kitaifa za kupambana na ukatili wa kijinsia.
Amesema mkutano huo unatoa fursa ya kutathmini mafanikio ya utekelezaji wa Ajenda ya Wanawake, Amani na Usalama, pamoja na kubainisha changamoto na mikakati mipya ya kuimarisha utekelezaji wake barani Afrika.

Dkt. Gwajima ameeleza kuwa licha ya hatua nzuri zilizopigwa katika kupanua usawa wa kijinsia, wanawake bado wanakabiliwa na vikwazo mbalimbali huku akitaja mila na desturi kandamizi, changamoto za kiuchumi na athari wanazokutana nazo wanawake wanaojitokeza kugombea nafasi za uongozi kuwa miongoni mwa mambo yanayopunguza ushiriki wao katika uongozi na siasa.

Amesisitiza kuwa utekelezaji wenye tija wa ajenda ya WPS unahitaji ushirikiano mpana kati ya serikali, mashirika ya kiraia, wadau wa maendeleo na taasisi za kikanda huu akisema Tanzania itaendelea kushirikiana na Umoja wa Afrika na wadau wengine ili kuhakikisha wanawake wanapata nafasi stahiki katika meza za maamuzi na michakato ya ujenzi wa amani barani Afrika.

Hata hivyo, ameonya kuwa teknolojia hiyo hiyo imekuwa ikichochea aina mpya za ukatili wa kijinsia mtandaoni, ambao waathirika wakubwa ni wanawake na wasichana.

Amefafanua kuwa mitandao ya kijamii imekuwa ikitumika kusambaza video za uongo, chuki, vitisho na matusi yanayolenga kuwachafua wanawake hadharani, jambo linalotishia usalama wao mtandaoni na kuwavunja moyo wanaotaka kushiriki katika uongozi na siasa.

Aidha amehimiza wadau wote kushiriki kikamilifu katika kutoa hamasa na elimu juu ya matumizi salama ya mitandao ili kulinda wanawake, wasichana na jamii kwa ujumla.

Dodoma, Tanzania – 12 Desemba 2025

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Mhe. Jenista Joakim Mhagama, kilichotokea jijini Dodoma.

Kupitia taarifa yake, Rais Samia amesema amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba huo mzito na kutoa pole kwa Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu, wananchi wa Jimbo la Peramiho, familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki.

Rais Samia amemuelezea Marehemu Mhagama kama kiongozi shupavu na mtumishi wa umma aliyejitoa kwa moyo wake wote kwa kipindi cha zaidi ya miaka 38 ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Katika safari yake ya kisiasa, Mhagama aliwahi kuwa kiongozi wa vijana, kiongozi wa wanawake, waziri katika awamu mbalimbali za serikali, pamoja na kuwa mshauri wa wanasiasa na wananchi wengi.

“Kwa miaka 38, Mheshimiwa Mhagama amekuwa mwanachama mahiri wa CCM, kiongozi wa vijana, kiongozi wa wanawake, waziri katika awamu mbalimbali na mnasihi wa wengi katika siasa na maisha,” amesema Rais Samia katika salamu zake.

Rais Samia amewaombea wafiwa faraja katika kipindi hiki cha majonzi na kumkabidhi marehemu kwa Mungu, akisema: “Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina.”

Mipango ya mazishi inaratibiwa kwa ushirikiano kati ya Serikali, Bunge na familia ya marehemu, na taarifa zaidi zinatarajiwa kutolewa.

 

Na Mwandishi Wetu

Mashabiki wa michezo na wakimbiaji nchini wanatarajiwa kujitokeza kwa wingi kwenye The SQF Zanzibar Cleft Marathon – Season 7, mbio maalum zinazolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto waliozaliwa na tatizo la mdomo na taya wazi (cleft).

Mbio hizo zimepangwa kufanyika Desemba 21, 2025 katika viwanja vya New Aman Complex visiwani Zanzibar, na zimekuwa kivutio kikubwa kwa wanamichezo, wadau wa afya, pamoja na wananchi wanaoguswa na masuala ya kijamii.

Kwa mujibu wa waandaaji, The Same Qualities Foundation (SQF), usajili kwa ajili ya mbio za mwaka huu umeshaanza katika maeneo mbalimbali ikiwemo New Aman Complex, Michenzani Mall, Forodhani, Masomo Bookshop, pamoja na Hospitali ya Edward Michaud jijini Dar es Salaam. Ada ya usajili ni shilingi 35,000 kwa washiriki wa mbio za 21KM, 10KM na 5KM.

Tukio hili ni zaidi ya mashindano, wamesema waandaaji. “Kila hatua unayokimbia ni sehemu ya kubadilisha maisha ya mtoto mmoja—kutoa tabasamu jipya, kuondoa unyanyapaa, na kurejesha matumaini kwa familia nzima.”

Mbio hizi zimepata pia heshima ya kuhudhuriwa na Mgeni Rasmi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, hatua inayoongeza uzito na hamasa kwa washiriki.

Kwa upande wao, wadau wa michezo wamepongeza juhudi za SQF kwa kuunganisha michezo na huduma za kijamii, wakisema mbio hizi zimekuwa mfano bora wa jinsi nguvu ya umoja inaweza kubadili maisha ya watu wanaohitaji msaada.

Waandaaji wametoa wito kwa wakimbiaji, klabu za michezo, mashirika na familia kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuchangia. Washiriki wanaweza pia kulipia kupitia M-Pesa kwa namba 5427230 (The Same Qualities Foundation).

Mbio hizi zinatarajiwa kuwa miongoni mwa matukio makubwa ya michezo ya kijamii mwaka 2025 nchini, yakileta pamoja wanamichezo, wafadhili na watu wa kada mbalimbali kwa lengo moja—kupigania tabasamu la mtoto.
Leo Desemba 9, tunapoadhimisha miaka 64 tangu Taifa letu lipate Uhuru, Tanzania Bloggers Network (TBN) inawapongeza Watanzania wote kwa kufikia hatua hii muhimu katika historia ya Taifa letu. Hii ni siku ya kutafakari safari tuliyotoka, mahali tulipo, na mwelekeo tunaoujenga kwa pamoja.

Waasisi wetu walituwachia zawadi kubwa—Uhuru. Lakini walituonya kuwa Uhuru hauwezi kuwa kamili bila kujitegemea. Leo tunakumbusha maneno ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyewahi kusisitiza:

"Uhuru hauwezi kukamilika pasipo kujitegemea. Hatuwezi kuitwa huru kama tunategemea wengine kutupatia mahitaji yetu ya kimsingi."

Tujenge Taifa Letu – Tusiibomoe Tanzania

Kama mtandao wa habari za kidijitali, TBN inasisitiza kuwa mafanikio yetu kama Taifa yametokana na utulivu, umoja na mshikamano. Ili kuendelea mbele, tunahitaji kudumisha amani na maridhiano—nguzo muhimu za maendeleo.

Rais mstaafu Benjamin William Mkapa alituasa kwa busara:

"Amani si kitu cha asili; tunahitaji kuilinda na kuitunza kila siku. Bila amani, hakuna maendeleo ya kweli."

Tukikubali kuongozwa na chuki, uchochezi na vurugu, juhudi za waasisi wetu za kupambana na ujinga, umaskini na maradhi zitapotea. Tusiitumie mitandao au uhuru wa maoni kuharibu Taifa letu; tuitumie kulijenga.

Kila Zama na Kiongozi Wake – Tuunge Mkono Mageuzi

Kila kizazi kina wajibu wake. Kama alivyoeleza Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi:

"Kila utawala na zama zake. Kila kiongozi na mchango wake katika ujenzi wa Taifa hili."

Katika awamu ya sasa chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tanzania inaendelea na mwelekeo wa 4R: Reconciliation, Resilience, Reforms, and Rebuilding. Huu ni mwaliko kwa Watanzania wote kushiriki katika kujenga Taifa lenye maridhiano, mageuzi chanya na uimara wa kiuchumi na kijamii.

Tuna nafasi ya kuzungumza—basi tuseme kwa njia inayojenga, si inayobomoa. Kuthamini Uhuru ni kufanya kazi kwa bidii, kulinda amani, na kuacha kutumiwa kuharibu misingi ya Taifa letu.

TBN Inawatakia Maadhimisho Mema ya Miaka 64 ya Uhuru!

Tanzania Kwanza — Kazi, Utu na Mshikamano. Tusonge Mbele!

Beda Msimbe
Mwenyekiti, Tanzania Bloggers Network (TBN)